Jumamosi, Septemba 12, 2015

Wanasiasa kuna maisha zaidi baada ya uchaguzi-Mwamalanga


Wiki hii Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima, ameibuka ndani ya vyombo vya habari ‘kumpopoa’ Katibu Mkuu wa Chadema, aliyejiondoa kwenye siasa kwa madai ya kupinga ujio wa Edward Lowassa ndani ya chama hicho. Hata hivyo Askofu Gwajima anampinga kuwa kilichomuondoa Chadema ni kupingwa na mchumba wake, aliyetaka awe rais naye apewe heshima ya mama wa Ikulu .
Kiongozi huyo wa kiroho, ameibua mambo mengi ambayo wapo wanaounga mkono hatua hiyo lakini kuna baadhi wanaoitafsiri kwa kuipa sura ya kidunia na si kiroho maana pengine kama kiongozi wa imani asingefanya hivyo. Pamoja na hisia hizo viongozi wenzake wa kiroho wanasema kutoka kwa ‘waraka wa Gwajima’ kuna cha kujifunza kama anavyoeleza Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kipentekoste, William Mwamalanga. (Pichani).

Mchungaji huyu anazungumza na Nipashe na kugusia baadhi ya mambo ya kukwepa ili kuepusha athari zaidi.
KUKASHIFU KANISA
Kama kiongozi wa kanisa anaelezea kukerwa na baadhi ya wanasiasa wanaosukuma tuhuma kwa viongozi wa dini wakiwahusisha na rushwa.
Mathalani kudai kuwa maaskofu wamehongwa kati ya Shilingi milioni 60 hadi 300 ili kumkubali mgombea mmojawapo, ni mambo yanayowafanya waumini kuwafikiria vibaya viongozi wao.
Anasema mbali na rushwa wapo baadhi ya wagombea na hata viongozi ndani ya jamii wanaohubiri siasa za chuki kuwa baadhi ya makabila ya Tanzania hawafai kuwa rais wa nchi hii.Kadhalika anasikitishwa na wagombea wanaodai kuwa upinzani unasababisha uvunjifu wa amani na hata kutumia mifano ya machafuko katika baadhi ya nchi za Afrika kuwa ziliamua kuua viongozi wao na sasa raia hao wanahangaika.
Anawataka Watanzania kufahamu kuwa kuna maisha baada ya uchaguzi. “Nataka kusisitiza kwa wanasiasa na Watanzania kwa ujumla wetu kuwa yapo maisha kabla na baada ya uchaguzi mkuu wa mwezi ujao.
“Ili amani yetu iendelee ni lazima tuache uongo, udini, utaifa wa kujibagua kwa mfano ‘ubara au uzanzibari’ hata ukanda kwani hiyo ndiyo mitaji ya kuangamiza taifa na wala siyo kuwa na wanachama wa upinzani.”
Anasema upinzani ni jicho la ziada la kukosoana na upo kikatiba na si mtaji wa kuvunja amani kama inavyodaiwa na baadhi ya wanasiasa. “Nawashauri wanasiasa kuwa upendo, amani , haki na wajibu wa kila mtu katika kutunza umoja ziwe kauli zenu.”
‘UONGO NI MATUSI’
Askofu Mwamalanga akizungumzia madai ya kuzuliana kama kupewa hongo na kusingiziana anasema kauli za uongo hazina tofauti na hotuba za matusi au kukashifu kwani zinahamasisha hasira ndani ya jamii hivyo kuwa chanzo cha vurugu na kuzalisha mitandao ya uovu jambo ambalo ni hatari kwa vile linatoa mwanya kwa maadui wa ndani na nje kujipenyeza na kuhatarisha umoja na amani ya nchi.
UVUMILIVU WA LOWASSA
Askofu Mwamalanga anamtaja mgombea wa urais kupitia umoja wa vyama vya Chadema, NCCR-Mageuzi, CUF na NLD Edward Lowassa, kuwa mfano wa uvumilivu wa kuigwa kwani pamoja na kuporomoshewa matusi, kulaumiwa na watu wengi kwenye kampeni amekuwa mtulivu na mwenye kulenga ujumbe anaotaka kuuwasilisha kwa wapiga kura.
Badala ya kutumia majukwaa kujibu matusi Lowassa amekuwa mtulivu na kutaka wale wenye ushahidi wauwasilishe, hivyo wanasiasa wengine wajifunze na huo ndiyo ustarabu wa kisiasa.
“Nawaomba wanasiasa muigeni Lowassa anafahamu kuwa kuna maisha kabla na baada ya uchaguzi.”
“Napendekeza baada ya uchaguzi mkuu itolewe tunzo ya utulivu au heshima wakati wa kampeni. Naamini kwamba hii itasaidia wagombea na wapambe wao kuwa watulivu wakati wote wa kampeni na baada ya uchaguzi Mkuu ili kulinda amani na utlivu wa nchi.”
VYOMBO VYA ULINZI
Anapozungumzia ‘jeuri’ ya Dk Wilbroad Slaa, kuwa analindwa na maofisa wa usalama wa taifa, anaona kuwa si jambo la kutamba kwa vile linatoa nafasi kwa watu kuwaza na hata kuzua mambo mengine ambayo hayaleti amani.
Anasema vyombo vya umma kama Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (Takukuru) na majeshi mengine yalinde umma siyo mtu binafsi.
Vyombo hivi ni muhimu  katika kusimamia haki na kuendelea kuwakumbusha wanasiasa na Watanzania kuhusu uchaguzi huku vikibeba jukumu la kuufanya umma uwe wa utulivu na amani kwa ustawi wa taifa.
Anaamini kiongozi wa siasa kutukana na kutoa tuhuma nyingi lakini pia akilindwa si jambo jema. Anawakumbusha Takukuru kuyafanyia kazi madai kuwa kuna rushwa imetolewa kwa vile Slaa anaweza kuwa ushahidi na kutibitisha au kukanusha tuhuma hizo.
Anaielezea hatua ya kuwatukana maaskofu kama kuporomoka kwa maadili kwani kumeambatana na matusi ,uongo na masingizio kuwa zaidi ya maaskofu 30 kati ya 34 wa Kanisa Katoliki wamehongwa kiasi kikubwa cha fedha.
Yapo maelezo mengine kuwa viongozi wa madhehebu mengine wamepewa rushwa na Askofu Josephat Gwajima, anaunganishwa na rushwa jambo ambalo lina lenga kuchafua kanisa na waumini.
“Hali ya kuporoka maadili ndani ya jamii na heshima kushuka miongoni mwa baadhi ya wanasiasa kunanilazimisha kukumbushana kuwa kuna maisha na urafiki baada ya uchaguzi mkuu wa mwezi ujao hivyo tunapaswa kuchunga kauli za vinywa vyetu ili kuepusha kuwa na maadui wa kisiasa na hata wa maisha yetu.”
Anaeleza kuwa kusema uongo dhidi ya watu fulani kunaweza kujenga uadui na kuhamasisha hasira ndani ya jamii hivyo kuwa chanzo cha vurugu na visasi si baina ya watu lakini hata miongoni mwa wanasiasa.
Anasisitiza kuwa kila jambo linaloonekana mbegu yake ni ‘mawazo’ ambayo huwa ‘maneno’, hivyo kuchunga ulimi ni jambo muhimu kuliko kingene chochote kwa kuwa kauli jambo linatokea. 
CHANZO: NIPASHE

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni