Jumatano, Agosti 05, 2015

Uandikishaji umekamilika, sasa tujipange kupiga kura.


Katuni.
Jana Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) ilikamilisha kazi ya kuandikisha wapigakura kwenye Daftari la Kudumu la Wapigakura kwa mfumo wa utambuzi wa kieletroniki wa kutambua alama za mwili (Biometric Voters Registration –BVT) kwa mkoa wa Dar es Salaam ambao ulikuwa ni wa mwisho katika uandikishaji.
Kazi ya kuandikisha wapigakura kwa mfumo wa BVR ilianza Februari 23, mwaka huu mkoani Njombe. 
Safari ya Nec iliyoanza Februari mwaka huu ilikuwa ni kuandikisha watu milioni 24 katika mikoa 31 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili wapate fursa ya kuchagua madiwani, wabunge na rais katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25, mwaka huu.
Tunaipongeza Nec kwa kuhimitisha kazi hii nzito na muhimu katika kuhakikisha kwamba wananchi wanatumia haki yao ya kidemokrasia kuwachagua viongozi wao kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka huu. Kila tukitazama nyuma, tunakumbuka changamoto nyingi ambazo Nec ilikumbana nazo. Hizi ni pamoja na kuanza kazi hiyo kwa kusuasua kutokana na uhaba wa BVR. Itakumbukwa kwamba awali Nec ilikuwa na BVR 250 ambazo zilikuwa zimenunuliwa wakati wa kazi ya uandishaji wa majaribio mwaka jana. Hadi kazi hii inamalizika jana, Nec ilikuwa na BVR 8,000 na zilisambazwa nchini kote, mkoa kwa mkoa. Ni jambo la kufurahi kwamba sasa kazi hiyo imekamilika.
Taarifa ambazo Nec imekuwa ikitoa kwenye mikoa mbalimbali ambako kazi hiyo ilikamilika, zinaonyesha kwamba mwitikio wa wananchi ulikuwa wa juu sana katika kujiandikisha. Kuna maeneo malengo yalivukwa kwa zaidi ya asilimia 100. Kazi nyingi nzuri zilifanyika. Sisi tunapongeza Nec kufikia mwisho huu mwema.
Hata hivyo, tungependa Nec iongeze uwazi na ushirikishwaji wa wananchi na wadau wote wa uchaguzi, kujua kiuhalisia ni watu wangapi wameandikishwa, orodha zitolewe kwa wakati jimbo kwa jimbo. Uwazi ndiyo jambo muhimu katika kufanikisha kazi hiyo. Nia ni kuepuka malalamiko na hata uwezekano wa kuwa chanzo cha vurugu kwenye uchaguzi.
Tunajua kwa hali ilivyo, itakuwa ni vigumu kuwa na muda wa kuhakiki daftari la wapigakura kwa maana ya kubandika majina yote ya waliojiandikisha katika vituo vya kujiandikisha kwa sababu ya muda. 
Ni jambo la bahati mbaya kwamba Nec imejikuta katika ratiba iliyobana sana ya kuandaa uchaguzi mkuu mwaka huu. Inajulikana dhahiri dhahiri kwamba uchaguzi ni mchakato, siyo upigaji kura pekee yake.
Uchaguzi huanza kwa uandikishaji wapigakura, uteuzi wa wagombea, ufanyaji wa kampeni, upigaji kura na kuzihesabu kwa uwazi na mwisho kutangaza matokeo. Huo ni utaratibu wa kisheria. Ni lazima uzingatiwe na kufuatwa pasi na kisingizio chochote.
Ni imani yetu kwamba Nec itaendelea kujibidiisha kuhakikisha kwamba hatua zinazofuata katika mchakato wa uchaguzi zinafanyika sawa sawa ili kujenga imani kwa wananchi kwamba weledi unawaongoza katika kazi hii muhimu ya kuhakikisha kwamba taifa hili linapata viongozi wanaotokana na ridhaa ya wananchi.
Tunajua kuwa hatua zilizobakia sasa kwa maana ya kuteua wagombea, kufanya kampeni, kupigakura na kuzihesabu na mwishowe kutangaza matokeo, ni muhimu sana. 
Ni kwa kutambua ukweli huo tunaamini kwamba Nec haitaiyumba katika kazi hii, itazingatia weledi, sheria na kanuni zote ili kufikisha mwisho mwema uchaguzi mkuu wa mwaka huu.
Kadhalika, tunaelewa kwamba hamasa walioyokuwa nayo wananchi kujitokeza kwa wingi kujiandikisha ni ishara ya kutambua haki zao na hivyo kuzitumia vilivyo ili ifikapo Oktoba 25, mwaka huu watumie vitambulisho walivyopata kuwachagua viongozi wao kwa njia ya kidemokrasia.
Tunawashauri na kwa kweli kuwachagiza, kwamba kujiandikisha ni jambo moja, lakini kupiga kura ni jambo la pili. Ni kwa jinsi hii tunawasisitiza wananchi kuwa watunze vema vitambulisho vyao vya kura ili wavitumie vema Oktoba 25, mwaka huu kufanya maamuzi juu ya nani anastahili kuwa diwani, mbunge na rais ili kuwaongoza kwa kipindi cha miaka mitano ijayo.
Haitakuwa jambo la kufurahi kama kujitokeza kwa wingi kiasi hicho kwa wananchi nia kuu ilikuwa ni kupata vitambulisho tu. Itakuwa ni jambo la faraja, la kuenziwa na linalojenga demokrasia na ushiriki mzuri wa wananchi katika kuamua mustakabali wa nchi yao kama watajitokeza kwa wingi kwa kasi na kiwango hicho hicho kupiga kura Oktoba 25, mwaka huu.
Tunawaomba wananchi watunze vitambulisho vyao na Oktoba 25, mwaka huu wavitumie kuamua nani awe diwani, mbunge na rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kipindi cha 2015-2020. 
CHANZO: NIPASHE

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni